Thursday, November 29, 2012

TAARIFA KUTOKA TFF LEO NOV 29,2012

Release No. 188
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Novemba 28, 2012
 
KILIMANJARO STARS YAPOTEZA MECHI YA CHALENJI
Tanzania Bara (Kilimanjaro Stars) imepoteza mechi ya michuano ya Kombe la Chalenji baada ya kufungwa bao 1-0 na Burundi katika mchezo uliofanyika leo (Novemba 28 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Mandela ulioko Namboole jijini Kampala, Uganda.
 
Bao hilo lilifungwa na Seleman Ndikumana dakika ya 52 kwa penalti. Mwamuzi Ronnie Kalema wa Uganda aliamuru adhabu hiyo baada ya Shomari Kapombe kumwangusha mshambuliaji huyo wa zamani wa Simba.
 
Washambuliaji wa Kilimanjaro Stars walilishambulia lango la Burundi kwa muda mwingi wa mchezo wakitafuta bao la kusawazisha. Hata hivyo mashuti ya John Bocco, Mrisho Ngasa na Amri Kiemba aliyeingia badala ya Simon Msuva ama yalitoka nje au kuokolewa na kipa Arthur Arakaza.
 
Akizungumza mara baada ya mechi hiyo, Kocha wa Kilimanjaro Stars, Kim Poulsen amesema ilikuwa ngumu hasa kutokana na uwanja kuwa na matope yaliyotokana na mvua iliyonyesha saa chache kabla ya kuanza mchezo huo wa kundi B.
 
“Katika hali ile ya uwanja ukifanya kosa ni ngumu kulifuta. Tuliruhusu penalti. Tulitengeneza nafasi nyingi, lakini kipa wa Burundi alikuwa kikwazo kikubwa kwetu. Katika mpira wa miguu ukishindwa kufunga unapoteza mchezo,” amesema Kim ambaye hii ni mara yake ya kwanza kuiongoza Kilimanjaro Stars kwenye michuano ya Chalenji.
 
Kilimanjaro Stars yenye pointi tatu baada ya kushinda mabao 2-0 dhidi ya Sudan katika mechi yake ya kwanza, itamaliza mechi za hatua ya makundi Desemba Mosi mwaka huu kwa kucheza na Somalia.
 
Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

No comments:

Post a Comment