Saturday, June 16, 2012

VIFO VYA WACHIMBAJI MADINI WADOGO NI UZEMBE

SIMANJIRO
Wachimbaji Madini Wadogo katika shughuli ya uokozi
Imebainishwa kuwa  vifo vinavyotokea kwenye machimbo ya madini ya Tanzanite Mji mdogo wa Mirerani Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara vinatokana na uzembe katika uchimbaji wa baadhi ya migodi hiyo.
 
Hayo yamebainishwa na Kamishna Msaidizi wa Madini Kanda ya Kaskazini Mhandisi Benjamin Mchwampaka kwenye mafunzo ya kuwajengea uwezo mameneja wa migodi yaliyofanyika ukumbi wa Kazamoyo Inn mjini Mirerani mkoani manyara..
 
Aidha aliongeza  kuwa tangu mwezi Januari hadi Mei mwaka huu wachimbaji wadogo 11 wamepoteza maisha kwenye machimbo ya migodi ya Tanzanite katika matukio tofauti.
 
“Matukio hayo ni vifo sita vya kuangukiwa na dunganya,vifo viwili kwa kukosa hewa au kuvuta hewa chafu migodini na kuteleza kwenye ngazi,kulipuliwa na baruti na kuangukiwa na mwamba kifo kimoja,” alisisitiza  Mchwampaka.
 
Alikemea vikali tabia ya baadhi ya wachimbaji wadogo kutumia baruti kama silaha badala ya kuzitumia kwa nyenzo za kazi kwa kuzifanya mabomu ya kienyeji na kuwalipua wachimbaji wenye migodi yenye uzalishaji.
 
“Serikali haitavumilia tena vitendo hivi na wote watakaohusika na jambo hilo mgodi wao utafungwa mara moja na tutafuta leseni zao kabla ya kuwachukulia hatua nyingine za kisheria,” alisema Mchwampaka.
 
Naye mwenyekiti wa Chama cha wachimbaji madini mkoa wa Manyara (Marema) Zephania Mungaya aliishukuru Serikali kutoa mafunzo hayo ambayo yatawanufaisha wachimbaji wadogo kupitia mameneja hao wa migodi.
 
“Napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa Serikali kwa kuandaa mafunzo haya ambayo yatazidi kuwajengea uwezo mameneja wa migodi ambao ndiyo daraja baina ya wamiliki wa migodi,wachimbaji na Serikali,” alisema Mughaya.   
 
Kwa upande wake Ofisa madini mkazi wa Mirerani Laurent Mayala alibainisha kuwa  lengo la mafunzo hayo ni kupunguza ajali migodini kwa kuwaongezea mbinu na elimu ya usalama na sheria ya madini ili kuboresha hali ya uchimbaji salama migodini.
 
Alimalizia kusema kuwa  mada zitakazotolewa ni usalama migodini,uzoefu na changamoto,sera na sheria ya madini,upelekwaji hewa migodini,matumizi ya baruti na tahadhari zake,wajibu na majukumu ya meneja na jiolojia ya miamba ya Tanzanite.     

No comments:

Post a Comment