Tuesday, January 3, 2012

KIBOKO APINDUA MTUMBWI NA KUMSHAMBULIA MVUVI ZIWA BABATI

Na:Mwandishi Wetu,Manyara
Mtu mmoja anayejulikana kwa jina la Ally Dengu (26) wa kijiji cha Bonga wilayani Babati  Mkoani Manyara  amefariki dunia  baada ya mtumbwi aliokuwa akiendesha kupinduliwa na mnyama Kiboko akiwa katika shughuli za uvuvi katika Ziwa Babati.
Mnyama Kiboko
 Kamanda wa Polisi mkoa wa  Manyara Lebaratus Sabas amedhibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa  tukio hilo limetokea siku ya tarehe 1 Januari mwaka huu majira ya saa 11 jioni ambapo marehemu alikuwa katika shughuli zake za uvuvi.
 Amewataka  wavuvi wa ziwa hilo kuwa  makini wakati wanapokuwa katika shughuli zao za uvuvi hata kama wanyama hao wamezoeana nao kwani huwezi kujua lini mnyama anabadilika kwa mfano kiboko anapokuwa amezaa huwa mkali.
 Kwa upande wake mwenyekiti za wavuvi wa ziwa hilo  Idd Hassan akiongea na Mwandishi wa  Blog hii Mkoani Manyara wavuvi hao wameiomba serikali kuwasaidia  ili kuweza  kuwapunguza viboko  hao kwani viboko hao wanaendelea kusababisha  adha kubwa kwa wavuvi pamoja na  wakulima wanaolima kando kando ya ziwa hilo.
 Ameongeza  kuwa forodha hiyo ya mbalakuu ndio kubwa kuliko zote katika ziwa Babati na ndio tegemeo la usambazaji wa samaki ndani ya mji wa Babati na nje ya mji huo  hivyo Halmashauri inapaswa kuwajali wavuvi wa eneo hilo kwa kuwahakikishia usalama wa kutosha
 Wakati huo huo  Issa Saidi ambaye pia ni mvuvi na shuhuda wa tukio hilo amesema  kuwa  ilikuwa majira ya saa 11 za jioni wakiwa Ziwani walimwona marehemu akishambuliwa na kiboko  na kwamba alipiga kelele za kuomba msaada lakini kwa kuwa mnyama huyo alikuwa karibu na marehemu wao walishindwa kumsaidia.
Takwimu zinabainisha kuwa  Katika mwaka 2011 pekee wamekufa  watu wanne kutokana na kuuwawa na viboko ambao wamekuwa wakiwashambulia wavuvi wakiwa katika shughuli zao za uvuvi ambapo  wavuvi hao walishapeleka malalamiko yao kwa viongozi wahusika lakini mpaka sasa hakuna kiboko aliyeuwawa au kudhibitiwa.

No comments:

Post a Comment